Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Wednesday, May 20, 2009
NIMETIMIZA WAJIBU WANGU

Mwaka sasa umepita tangu nianze safari hii ya kusaka elimu niliyoamini ni muhimu sana kuipata kuliko kuikosa. Nashukuru katika mwaka huu nimekabiliana na mengi na kutokana na hayo naweza sasa kusimama kuwa nimebadilika.

Maisha ya binadamu yana fasili nyingi, yaweza kuwa yale ya kukumbatia sifa mbazo hazikujengi ama kukumbatia watu walio na sumu ya kukuua. Maisha haya haya yaweza kuwa yale ya kuwa na wasiokuthamini ama kuwa na wanaokuthamini. Yote haya ni maisha na ni vigumu kwa mtu kufahamu nani ni nani katika maisha yake.

Ni katika njia hii sasa naweza kutambua maumivu yangu yamepoozwa na nani na akina nani walitegemea kufurahia mimi kubakia katika maumivu! Pia naweza kutegua kitendawili kuhusu nani waliweza kukaa name wakati nikihitaji kuw anao zaidi.

Kwa ujumla kazi niliyofanya nafahamu baadhi hawakupenda kuona nikiifanya lakini wapo walionipa nguvu siku zote kwa kile kisemwacho: “binadamu wengi hupenda kuona ukishindwa jambo ili waibuke na kusema, tulijua tu ataanguka.” Katika wanaoamini katika falsafa ya kushindwa kwangu wamekosa nafasi!

Maisha mapya yanakuja baada ya safari hii. Ndugu zangu akina Materu na Msangi kama sio Mwaipopo watafahamu pia namna nilivyokimbiza mpira huu hadi kuuweka katika penati. Nimepiga penati hii leo japokuwa huwezi kubaini ni lini gori litaingia lakini hadi sasa mpira upo katikati ya gori na kipa namuona anaelekea kushindwa kuuzuia.

Kikubwa ni kuwa, hakuna atakayekushika mkono kuingia darasani katika ulimwengu wa leo. Hakuna atakayekuhamasisha kusoma kwa kuwa anafahamu kwa kufanya hivyo unakaribisha uhuru na ukombozi wako. Adui mkubwa wa maisha ya mtu ni yeye mwenyewe hasa anapokubaliana na hali dhaifu na kuikumbatia kwa kusema, 'nitafanyaje'!

Mwisho nimshukuru Jalia kwa nguvu zake nyingi na majaribio mengi aliyoyapitisha shetani katika kipindi hiki cha mwaka mmoja. Ni kweli navunja rekodi katika Chuo hiki kwa kuwa mwanafunzi wa kwanza kukamilisha masomo haya katika Shule ya Serikali kwa muda wa mwaka mmoja. Hii ni faraja kwangu, nimeandika historia katika uwanja mwingine. Nafahamu njia inayonikabili kuanzia kesho ni ngumu lakini nimejiandaa vema kukabiliana nayo kuliko unavyodhani.
 
© boniphace Tarehe 5/20/2009 12:58:00 AM | Permalink | Maoni 8
Sunday, March 22, 2009
HII NDIYO SURA HALISI YA AFRIKA

AFRIKA ni bara linaloongoza kwa kuwa na sura za umaskini hasa ule unaowafanya binadamu kukosa kile alichokiita Abraham Maslow haki za msingi yaani chakula, malazi na mavazi. Nimepita hapa na kukuta taarifa na picha hii ambayo kwangu haijanifurahisha.

Haki chakula ni jambo ambalo nimekuwa nikilizungumza sana na ninatamai siku moja kila mwananchi kwa kuanza na Tanzania apate haki hii ya msingi. Kama tukikubali kurejesha sera za vitendo katika kilimo bila shaka tutamudu kuwezesha watu wetu kupata chakula wakati wote.

tunafahamu kuwa wakishapata chakula kiasi cha kushiba ni jukumu la pili kusisitiza juu ya chakula bora. Wimbo wa chakula bra hauwezi sasa kuimbw ana serikali yetu kwa kuwa hata haki ya chakula tu kwa wananchi bado ni kitendawili. Kuna waziri wa Kilimo nchini anaitwa Wassira, ni maarufu sana kwa maneno matamu lakini utendaji wa wizara hiyo katika kutibu tatizo la upatikanaji wa chakula bado ni ndoto takayohukua siku nyingi kupata jibu. Tunasubiri sijui aje nani ili kuhamaisha kilimo cha chakula katika Afrika? Inakera na kuumiza sana!
 
© boniphace Tarehe 3/22/2009 07:21:00 AM | Permalink | Maoni 6
Wednesday, March 18, 2009
HUU NI UZANDIKI

KITENDO cha wakubwa kujilipa bonasi ya $165 billioni wakati wamekomba fedha ya serikali $ 170 billioni ni fedheha na aibu katika ulimwengu unaomilikiwa na soko. Dhana ya kuwaacha wenye nguvu washike mpini kama walivyokuwa wakiachiwa na Bush haina haja kupingwa kwa nguvu zote. Hili ndilo linalotakiwa kufanyika hata kwa serikali maskini na sio kutazama tu watu wenye fedha nyingi wanajitoza kodi kwa kutumia mbinu za misaada huku wakinufaika na kutokatwa kodi kwa kigezo kuwa wanashiriki shughuli za umma. Obama anaonyesha njia sahihi katika hili pia. Habari zaidi soma hapa na pichani ni Treasury Secretary Timothy Geithner
 
© boniphace Tarehe 3/18/2009 12:16:00 AM | Permalink | Maoni 1
Tuesday, March 10, 2009
NIMESHINDWA KUTIMIZA AHADI
JUMAPILI iliyopita ilikuwa siku ya Wanawake Duniani. Siku hiyo ni muhimu sana kwangu na nilidhani kupitia eneo langu nizungumze machache. Akina mama hasa wa Afrika wanapitia vipindi vigumu mno katika maisha yao hasa sasa ambapo tabia za wanaume wengi kuanza kujiingiza katika tamaduni za magharibi.

Hali ya kuwathamini akina mama ambayo utamaduni wa Kiafrika ulikuwa ukifafanua sasa iko katika hatihati. Na akina mama nao wengi wameingia katika mtego wa kutotambua kuwa maisha yao ambayo ni ya muhimu sana katika dunia ynahitaji uvumilivu ambao wamezaliwa nao na kweli wanaumudu.

Nilijiwekea ahadi ya kuzindua kitabu katika siku hii; Kama wakumbuka chaitwa 'Barua kwa Mama' lakini bado sijafanikiwa kufanya hivi. Hata hivyo msomaji Barua kwa Mama ipo katika hatua njema; wakati ukifika itatoka. Binafsi siamini katika utunzi wa kukimbizana maana kazi za sanaa hazifi na ndio maana kila nisomapo muswada huu najikuta nacheka kwani unabeba kauli na maarifa ambayo yanaweza kuishi kwa miaka mingi zaidi. Salamu kwa akina mama wote.
 
© boniphace Tarehe 3/10/2009 03:18:00 AM | Permalink | Maoni 1
Friday, October 31, 2008
NIPO NAISHI DAR
NI siku nyingi sijaingia hapa, wengi wamehoji haka kaukimya nimekaanzishia wapi. Nikajiuliza tena binafsi nimelala wapi? Lakini kuna kubwa moja, ukimya una mafunzo makubwa na unamkuza mtu akitaka kufanya tafakari. Nikionacho katika maisha yangu ni furaha, nawatazama watu wengi wakianza kuishi furaha hii. Wengi niliwapoteza lakini sasa wanaanza kurejea kwa kasi mno.

Maisha yangu yanakuwa huru kiasi, nakosa makundi ambayo yalianza kujijenga. Lakini kuna ndoto zinazoingia na kutoweka. Moja ni hii ya siasa! Siasa jambo baya maana lahusisha mbinu mbaya na chafu. Kuna kundi limeingiza mbinu zisizoonekana katika kuweka mambo sawa katika siasa, lakini binafsi naamini sasa katika siasa elimu.

Nina jukumu mbele yangu na hii ni safari ya kutafuta PHD nikiifanikisha safari hii nitafarijika sana. Nitafurahisha moyo wangu maana ni jambo ambalo nimekuwa nikilipenda sana na hata Mzee Benjamin Makene amekuwa akishangilia kuhusu wazo hili. Najua nitakuwa na jukumu la familia maana mimi si kiumbe wa kuwepo kuwepo tu. Nitalizungumzia hili siku zijazo maana hapa ndio kasrini kwangu, ambapo sasa pia panachapishwa katika gazeti la Rai na nategemea hata nyumba yangu kuwa na jina hili. Nishukuru kurejea kwa staili hii, nijipe moyo maana kuwepo na kuondoka zote ni faraja na mikakati ya Jalia.
 
© boniphace Tarehe 10/31/2008 03:47:00 AM | Permalink | Maoni 3
Monday, November 26, 2007
Hofu kuhusu kamati ya madini inatoka wapi?

MICHAPO kama kawaida mingi sana katika Tanzania. Juzi nimefarijika kukutana na ndugu ambao nimeachana nao siku nyingi.

Kama kawaida majadiliano yetu yakabaki kuzungumzia habari kavu. Sipendi mijadala ya mambo mazito kila mara. Natamani nikutanapo na rafiki watambue hili lakini wao ndio kama kwao kumepambazuka!

Ukifika tu baada ya salamu, kinachofuata ni mambo mazito. Mijadala kuhusu mustakhbari wa Tanzania. Mijadala kuhusu madini na vinginevyo.

Binafsi naamua kuwahamishia katika hoja ya kilimo. Natamani kila mmoja azungumzie kilimo maana ndicho kinachoweza kuleta tija hapa Tanzania.

Kilimo kikiwekewa mkakati wa dhati ni wazi tutarejea katika harakati za kusaidia nchi kujikwamua katika tatizo la kukosa chakula. Kilimo pia chaweza kutusaidia kama taifa kurejesha mkakati wa kuhamasisha chakula bora.

Faida za chakula bora kwa wananchi ni pamoja na kujenga afya zao, huku pia kukiwa na faida ya kuwezesha akili kuwa tulivu na hivyo mtu kuwa makini katika utendaji wa mambo anayotakiwa kufanya.

Wakati nikiwa na tafakari za kilimo nakutana na mwanafunzi mmoja wa Chuo Kikuu Mlimani. Huyu msomaji wa safu hii na ananipachika swali kuhusu hali ya wanafunzi kwa wakati huo.

Anachokieleza ni kuwa nchi haiongozwi tena vema. Nchi imebakia mfano wa kundi la wajanja wachache ambao wamekutana kunywa kahawa. Namuuliza yeye angetaka iweje?

Ananitazama na kuanza kutoa mada! Sina muda wa kukaa hapo alipo na kubwa ni hili la kuchoka kujadili mada ngumu na mambo mazito mazito kila siku.

Mwaka unaisha, unakuja mwingine na ukifanya tathmini utabaini kuwa kichwa kinahitaji kusikia habari tulivu. Kinahitaji kuchekeshwa maana yaelezwa kucheka ni tiba kwa binadamu.

Kichwa hakitaki kusikia habari za huzuni tu. Kinataka pia kusikia vituko na purukushani zingine za dunia. Kinahitaji kupata taarifa zitakazoweza kukupanga kimkakati ili uzidi kufanikiwa na kuirejeshea jamii.

Kutokana na hilo nimeamua kuvuta hewa, nimeamua kupumzika kiasi, lakini kosa la kazi hii siwezi kukimbia na kuacha kasri hili bila chakula.

Wapo wanaoweza uliza mbona nilikimbia katika Gazeti Tando! Jibu lipo dogo tu, navuta pumzi ili nirejee tena. Siku si nyingi nitakuwa huko pia.

Kama ambavyo sasa naamua kujadili kuhusu utata wa Kamati ya Madini iliyoundwa na Rais Kikwete. Usishangae kunikuta nami najiingiza katika mjadala wa kamati hii.

Sina utaalamu kuhusu madini lakini naweza kujadili kamati. Kamati imeundwa na tayari ukitazama yameanza kuibuka mambo.

Jambo kubwa ni watu waliowekwa katika kamati hiyo. Siku moja baada ya kamati hiyo kusomwa, mmoja wa wajumbe sidhani hata kama alikuwa kapata barua rasmi ya kuwa mjumbe wa kamati, alisikika akikubali kwa moyo mkunjufu uteuzi wake.

Siku mbili baadaye kauli kutoka chama chake zikaanza kukinzana na kukiri kwake. Sasa kunaelezwa kuwepo kwa watu wasiopaswa kuteuliwa katika kamati hiyo. Hii ndiyo Tanzania ambayo kila jambo unalofanya linatakiwa kupindishwa hata kama faida au hasara yake hii wazi.

Wanasiasa wanaishi kimtego mtego. Kazi yao ni kutegana na inapogundulika kuwa mmoja anataka kuzidi kete utaona mwingine akiibuka na kulalamika. Hapa ndipo unapotazama sasa hoja ya kamati ya madini inapoanza kupoteza maana ya kazi yake na sasa kazi inageukia kutazama watu wanaounda kamati hiyo.

Mwisho wa siku kamati itafanya kazi na inavyoonyesha majibu ya kamati hii huenda yasipewe maana, kwa kuwa makundi yamejigawa tayari kusubiri majibu wanayoyapenda!

Wiki iliyopita nilidodosa kiasi kuhusu wajibu wa wajumbe wawili kutoka upinzani. Nilidodosa pia wasifu wao huku nikimuelezea Cheyo John kama mwanasiasa mwenye uwezo wa kuunganisha nguvu za pande zaidi ya chama chake.

Mwingine Zitto Kabwe sikumjadili maana kwa maisha na umri hajaweza kujenga tabia ya jumla ya kumbainisha alivyo katika siasa. Lakini sasa hivi ni maarufu na hasa katika hoja za madini.

Ni humo alimoingizwa huku kukiwa na tetesi mtaani kuwa, kama hakufanya tafiti vema katika hoja zake alizozitoa miezi kadhaa kwa sasa anaweza kuwa katika nafasi ya kulamba matapishi!

Hili linaweza kuwa hofu ya chama chake ambacho kimeanza kuhoji baadhi ya majina katika kamati hiyo. Lakini kwa nini tusisubiri majibu ya kazi hiyo na kuiacha kamati kufanya kazi yake kwanza?

Hofu ya aina hii ina picha ya sura za wanasiasa! Sura zao hugeuka kila mara, leo watataka hili na kesho wakiliona linakuja katika njia nyingine ya kuwaathiri wanakimbia! Huenda Chadema kimeshaona jambo lililojificha na kama ndivyo, chama hiki kinatakiwa kutambua mbinu nzuri kuliko hii ya sasa ya kuanza kuufanya umma utazame wanaounda kamati badala ya kazi ya kamati.

Kinachofanywa sasa ni kuonyesha kuwa kamati hiyo haitafanya kazi, ama itafanya kazi lakini kwa upande ule ule wa kuvutia kwa serikali. Lakini si kuna wajumbe wa upinzania ndani ya kamati hii? Kama ndivyo, tuamini kuwa Tanzania kuna wapinzani wa majina tu?

Kama kawaida jamii inaanza kuchanganywa hali itakayofanya mwisho wa siku tusibaini kama kulikuwa na ulazima wa kuiunda kamati hiyo, kufuatia pia kuwepo kwa kamati za madini zaidi ya tatu huko nyuma. Hofu hii inatoka wapi na nani anatakiwa kunufaika na hofu hii? Wanasiasa wana maisha magumu na yasiyotabirika! Naamini wanaweza hata kutoa majibu ya hofu yao ila la msingi tunataka ukweli kuhusu utata huu wa mambo ya madini nchini.


 
© boniphace Tarehe 11/26/2007 12:46:00 AM | Permalink | Maoni 3
Friday, November 23, 2007
NIPO
KATIKA harakati za kutoka kuzimu mimi Boniphace Makene natangaza kurejea duniani humu. Safari yangu ya kuzimu ilikuwa ndefu na hadi narejea hapa nina uchovu mwingi. Sitarajii kuwa kuzimu karibuni lakini nimejifunza mengi katika safari yangu hiyo.

Nimejifunza kuhusu kuingia zama mpya ambazo zinaweza kuwa hatari kwa maisha ya watu wengi. Nimejifunza utamaduni mpya wa watu kuvuana nguo bila kupenda. Nimejifunza na kujifunza na taarifa nyingi nitazungumza nanyi siku zijazo.

Nitumie fursa hi kuomba radhi kwa wale ambao sikuwaaga wakati nachukua maamuzi ya kusafiri safari hiyo. Nimerejea ndugu zangu na kama niko salama nadhani mnaweza kuona. Niishie hapa maana bado nina uchovu. Karibuni katika Kasri lenu ambalo mmelitunza hata wakati nikiwa safarini.
 
© boniphace Tarehe 11/23/2007 11:41:00 PM | Permalink | Maoni 2
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved